DAR ES SALAAM:
Na Mwandishi Wetu
Imamu Mkuu wa Msikiti wa Manyema na Mjumbe wa Baraza la Ulamaa la Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Taifa, Sheikh Hamid Masoun Jongo, amewataka Watanzania, hususan vijana, kuwa
waangalifu na mbinu zinazolenga kuchochea machafuko kuanzia mwezi Mei 2026
kupitia maandamano yasiyo na kikomo. Amesema amani haina mbadala na ni wajibu
wa kila mwananchi kuilinda ili iwe urithi kwa vizazi vijavyo.
Sheikh Jongo ametumia fumbo la
"Panya na Almasi" kuelezea hatari ya vijana kutumika kama vyombo vya
kubeba madai ya haki kwenda kwa watu anaowaita maadui wa nchi. Ameeleza kuwa
katika mazingira hayo, vijana wanaweza kuangamia huku rasilimali za nchi
zikichukuliwa na wahusika wa nje bila gharama.
Amehoji uhalali wa kauli ya
"bila haki hakuna amani," akisema kuitangaza Tanzania kuwa haina haki
ni kuishutumu nchi na wakazi wake. Sheikh amewataka vijana kutumia muda wao
kusoma na kuelimika badala ya kuingia kwenye mikumbo ambayo huko nyuma
ilisababisha vifo na majeraha kwa raia.
Katika hotuba hiyo, Sheikh amepongeza
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa hatua za serikali kufungua milango ya elimu
na teknolojia kwa vijana. Amesema mfumo huo unalenga kuwaandaa vijana kurithi
uongozi wa nchi kwa weledi na maarifa.
Vilevile, Sheikh amedai kuwepo kwa
njama zinazolenga kuzuia mashindano ya mpira wa miguu ya AFCON kufanyika
nchini. Amesema michezo ni fursa kwa vijana na chuki za kisiasa zisiruhusiwe
kuharibu mipango ya maendeleo ya michezo.
Amebainisha kuwa utulivu uliopo ndio
uliowezesha utekelezaji wa ibada za mwezi wa Ramadhani na sala za Tarawehe bila
vikwazo. Amesema mwananchi anaposhukuru kwa amani iliyopo, anajenga msingi wa
kupata utulivu zaidi.
Sheikh amesisitiza kuwa sekta ya
utalii na kumbukumbu za kitaifa haziwezi kuwepo bila amani, jambo
litakalosababisha mdororo wa kiuchumi. Ameeleza kuwa amani ikivunjika, athari
zake huenea hadi ndani ya nyumba za raia na kuondoa utulivu wa kila mmoja.
Amewataka wananchi kushikamana na
kuwaombea viongozi wa nchi ili waendelee kuiongoza Tanzania katika misingi ya
amani na utulivu. Amesema Tanzania ni mali ya wote na kila mkazi anaihitaji
amani kwa ajili ya shughuli zake za kila siku.
Mwisho, Sheikh ametoa wito kwa wale
wanaopanga kuvunja amani kuacha mipango hiyo. Amesisitiza kuwa jamii imejifunza
kutokana na matukio ya nyuma na haitakubali kuruhusu vurugu ziharibu mfumo wa
maisha uliopo.
